Imeandikwa na Pety Siyame, Mpanda
MAHAKAMA ya Wilaya ya Mpanda mkoani Katavi imemhukumu mkazi wa Kijiji
cha Sibwesa katika Wilaya ya Tanganyika, Peter Ngomalala (50) kifungo
cha maisha baada ya kutiwa hatiani kwa kosa la kumbaka mtoto wa kike
mwenye umri wa miaka tisa, mwanafunzi wa darasa la pili katika shule ya
msingi wilayani Tanganyika huku mtoto mwenzake wa kike mwenye umri wa
miaka saba akishuhudia.
Hakimu Mkazi Mfawidhi wa mahakama hiyo, Chiganga Ntengwa alisoma
hukumu hiyo jana alisema ameridhishwa na ushahidi wa upande wa mashtaka
bila kuacha shaka kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo.
Upande wa Mashtaka ukiongozwa na Wakili wa Serikali, Flavian Shiyo
uliwaita mashahidi kadhaa akiwemo mtoto huyo aliyebakwa na pia mama yake
mzazi. Hakimu alisema mshitakiwa alitenda kosa hilo kinyume cha kifungu
cha Sheria namba 130 (1)(2) na kifungu cha Sheria 131 (3) kanuni ya
adhabu.
Alisema mtoto mwingine aliyeshuhudia na aliyebakwa wote pamoja na
kuwa na umri mdogo, bado walitoa ushahidi kwa ufasaha ambao haukuacha
shaka yoyote kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo.
Hakimu alisema mahakama hiyo ilijiridhisha na ushahidi wa muuguzi wa
zahanati ya Sibwesa mtoto huyo alikofanyiwa uchunguzi wa kitabibu na
kupewa dawa za kufubaza makali ya Virusi vya Ukimwi (ARVs).
Awali Mwendesha Mashtaka, Wakili wa Serikali, Shiyo alidai mshtakiwa
alitenda kosa hilo Oktoba 12, 2016 saa 4 asubuhi kijijini Sibwesa ambapo
alimkuta mtoto huyo akicheza na mwenzake jirani na kwao akawalaghai
watoto hao wamfuate nyumbani kwake akawape fedha wanunue biskuti na
vinywaji baridi.
Wakili Shiyo alidai kabla hajafika nyumbani kwake alimvuta mtoto huyo
kwa nguvu na kumpeleka eneo la tangi la maji na kumbaka huku mwenzake
akishuhudia tukio hilo na licha ya watoto hao kupiga kelele za kuomba
msaada hakumwachia.
Ilidaiwa watoto hao waliwataarifu wazazi wao ambako mshtakiwa alitiwa
nguvuni na askari mgambo wa kijijini humo na kumfikisha katika kituo
cha polisi. Mshitakiwa alijitetea akidai hakumfanyia mtoto huyo unyama
huo, bali mama yake mzazi amemsingizia kwa kuwa alikuwa akimdai fedha
alizomkopesha hivyo kuomba mahakama imwachie huru.
CHANZO HABARI LEO
0 comments:
Post a Comment