Imeandikwa na Pety Siyame, Sumbawanga
MAHAKAMA Kuu ya Tanzania, Kanda ya Sumbawanga imewahukumu ndugu sita
wa familia moja kunyongwa hadi kufa baada ya kutiwa hatiani kwa kumuua
kwa kukusudia ndugu yao Raymond Kamande wakimtuhumu kuwa mchawi.
Wanandugu hao ambao ni wakazi wa kijiji cha Mkoe wilayani Kalambo
wanadaiwa usiku huo wa tukio wakiwa na fimbo, fyekeo, mapanga na mashoka
walivamia na kuteketeza nyumba ya ndugu yao huyo kwa moto kisha
wakamuua na mwili wake wakauchoma moto.
Waliohukumiwa kifo na mahakama hiyo ni pamoja na Peter Mpandashalo,
Aristed Kamande, Stephan Sikanda, Herric Nguvumali na Anatory Kamande.
Aidha mahakama hiyo iliwaachia huru ndugu wawili Wilbroad Kamande na
Aristed Kamande.
Akisoma hukumu hiyo, jaji wa mahakama hiyo, Dk Adam Mambi alisema
washitakiwa hao sita walitenda kosa hilo kinyume na kifungu 199 cha
makosa ya jinai Sura ya 16 kama ilivyofanyiwa mapitio mwaka 2002.
Upande wa mashtaka uliongozwa na Wakili wa Serikali, Scholastica
Lugongo akisaidiwa na Adolf Lema waliwaita mashahidi sita kuthibitisha
bila kutia shaka ushahidi wao dhidi ya uhalifu uliofanywa na washtakiwa.
Awali wakili wa serikali, Lugongo alieleza mahakama hiyo kuwa
watuhumiwa hao kwa pamoja walitenda makosa hayo Septemba 27, mwaka 2014
katika kijiji cha Mkoe wilayani Kalambo.
Ilidaiwa mahakamani hapo kuwa usiku huo wa tukio washtakiwa hao sita
wakiwa na silaha za jadi walivamia nyumba ya ndugu yao Raymond kijijini
hapo akiwa amelala humo na kuiteketeza kwa moto.
Kwa mujibu wa Wakili Lugongo, Raymond katika jitihada za kujiokoa
alipenya kwenye dirisha la chumba chake lililoanguka na kukimbilia
kujificha kwenye nyumba ya mtoto wake wa kiume, David Kamande.
CHANZO HABARI LEO
0 comments:
Post a Comment