Home » » POLISI WANAO NYANYASA MAHABUSU WAADHIBIWE

POLISI WANAO NYANYASA MAHABUSU WAADHIBIWE

SIKU zote tunaamini Polisi wako kwa ajili ya kulinda na kuhakikisha usalama wa raia. Hata hivyo dhana hiyo huenda ikaanza kuleta utata hasa kutokana na matukio ya ukatili yanayohusisha polisi kuongezeka kila wakati.
Matukio mengi ya polisi kunyanyasa raia ikiwemo mahabusu yamekuwa yakiripotiwa katika vyombo vya habari, jambo ambalo linasikitisha na kutia huzuni sana, hasa ukizingatia kuwa watu wengi wamekuwa wakiamini kuwa polisi ndio kimbilio lao, sehemu ambayo haki na usalama vinaweza kupatikana.
Hata habari za polisi kunyanyasa mahabusu zimekuwa zikiandikwa ama kuripotiwa katika vyombo vya habari jambo ambalo kimsingi linatia doa jeshi hilo, zaidi kuleta woga kwa watu wanaojikuta wamevunja ama kukiuka Sheria na kujikuta mikononi mwa Polisi.
Kilichonisukuma hasa kuzungumzia hili ni tukio lililoripotiwa na vyombo vya habari kutoka Sumbawanga ambapo polisi wanane akiwemo mmoja wa kike kutuhumiwa kumtesa mahabusu mwanamke kwa kumvua nguo na kumuingizia chupa ya bia katika sehemu za siri.
Ukisoma habari hii, kama una moyo mwepesi sana unaweza usimalize kuisoma kwani inaogofya na kusikitisha kuona binadamu anavyoweza kubadilika na kuwa katili kwa binadamu mwingine kwa kiwango cha namna hii.
Lakini cha kuogofya zaidi ni vitendo hivyo kufanywa na polisi ambao wamepewa jukumu la kulinda na kuhakikisha usalama wa raia wake haijalishi mtu huyo ni mkosaji kiasi gani, kwani ndio maana kuna Mahakama ambazo zinajukumu la kusikiliza kesi na mwisho kutoa hukumu kwa mtuhumiwa.
Kitendo cha mshtakiwa aliyetajwa kwa jina la Clara God kufanyiwa unyama huo na polisi ni kitendo cha unyanyasaji na ukatili wa kutisha ambao naamini hakipaswi kufumbiwa macho. Mtuhumiwa huyo na wenzake watatu wa kiume wanakabiliwa na kesi ya unyang’anyi wa kutumia silaha na wako rumande kwa kuwa kesi yao haina dhamana.
Akizungumza mbele ya Hakimu Mkazi wa mjini Sumbawanga, Rosalia Mugissa, mshitakiwa Clara akibubujikwa na machozi alieleza namna askari Polisi walipofika nyumbani kwake katika Kitongoji cha Chanji na kumtaka aeleze alipomficha mumewe na kisha kumchukua kwa nguvu na kumbambikia kesi hiyo ya unyang’anyi wa kutumia silaha.
Kisha mtuhumiwa huyo ndipo alipoeleza unyanyasaji na kitendo cha ukatili alichofanyiwa na askari hao, kwa kudhalilishwa kwa kuvuliwa nguo na kisha kulazimishwa kukalia chuma na machungu aliyopitia mwanamke huyo.
Ninachoamini polisi wana njia nyingi za kulazimisha mtuhumiwa kusema ukweli au kukiri makosa lakini vitendo vya namna hii havipo katika taratibu hizo, huu ni ukatili ambao viongozi wa Jeshi la Polisi wanapaswa kuvifuatilia, kuvikemea na kuvikomesha kabisa.
Vile vile bado ninaamini hawa ni baadhi ya polisi ambao hawana ubinadamu, utu na maadili na ndio wanaochafua Jeshi la Polisi na kufanya watu waone kama polisi ni watu waliojaa ukatili wakati wako polisi wengi wanofahamu wajibu wao wa kulinda raia na haki zao.
Ninachojiuliza unapomfanyia mtu ukatili wa namna hii, halafu baadaye ikabainika kuwa hana kosa lolote, unajisikiaje? Najikuta nikijiuliza, hivi kwenye Jeshi letu la Polisi watu wanaoajiriwa wengine ni majambazi au ni wauaji, nashindwa kupata jibu la haraka maana kwa akili za kawaida unashindwa kuamini polisi mwenye maadili na aliyesomea wajibu wake vizuri anaweza kuwa katili kiasi hiki.
Ninachoelewa hata mahabusu au mfungwa ana haki yake kama binadamu mwingine yoyote na hastahili wala hapaswi kufanyiwa ukatili wa namna hii hata kama amefanya kosa kubwa kiasi gani.
Kuna haja sasa ya viongozi wa Polisi kufuatilia polisi wake kwa umakini ili wale watakaobainika kuwa na mambo yasioeleweka waondolewe mapema, badala ya kuacha waendelee kuwanyanya na kutesa watu kwa kiwango cha namna hii na kuchafua jeshi hilo kwani inasikitisha na inahuzunisha.
Chanzo;Mwananchi
Jika Anda menyukai Artikel di blog ini, Silahkan klik disini untuk berlangganan gratis via email, dengan begitu Anda akan mendapat kiriman artikel setiap ada artikel yang terbit di Creating Website

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Rukwa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa