Sumbawanga. Watu wawili wanaosadikiwa ni
majangili wametelekeza begi moja likiwa na vipande saba vya pembe za
Tembo, vyenye uzito wa kilo 19 vikiwa na thamani ya zaidi ya Sh45
milioni.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Katavi, Dhahiri
Kidavashari alisema tukio hilo lilitokea Desemba 24, mwaka jana saa
2:30 usiku Kijiji cha Kabungu, barabara inayotoka Mpanda kuelekea
mkoani Kigoma.
Kidavashari alisema siku ya tukio polisi
waliokuwa doria waliwaona watu hao wakiwa wamepakia beji kubwa jeusi
kwenye pikipiki aina ya SanLg, waliwatilia mashaka watu hao na kuanza
kufuatilia nyendo zao.
Alisema wakati wakifuatilia walipata taarifa za
raia wema kwamba, watu hao walikuwa na nyara za Serikali kinyume cha
sheria hivyo jitihada za kuwanasa zilianza kwa kuandaa mtego.
Kidavashari alisema polisi waliokuwa wameandaa mtego wa kuwakamata, watuhumiwa waliposimamishwa waligoma.
Alisema hali iliyolazimu polisi kuanza kuwafukuza,
walipogundua wanafuatwa na askari waliacha njia na kuingia kwenye
kichaka na kutoweka huku wakitelekeza begi jeusi ambalo lilikuwa na
vipande hivyo vya pembe za Tembo na pikipiki waliyokuwa wakitumia.
Kamanda Kidavashari alisema baada ya polisi
kufanya upekuzi kwenye beji hilo, walikuta vipande saba vya pembe za
Tembo vyenye uzito wa kilo 19 vya thamani hiyo ya fedha.
Chanzo;Mwananchi
Chanzo;Mwananchi
0 comments:
Post a Comment