Home » » MTOWISA WAZUIA MKUTANO WAKIDAI GARI

MTOWISA WAZUIA MKUTANO WAKIDAI GARI

WAKAZI wa Kata ya Mtowisa wilayani Sumbawanga, Rukwa wamewakatalia madiwani sita wakiongozwa na Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya hiyo kufanya mkutano wa hadhara kwenye eneo lao wakishinikiza gari la wagonjwa lirejeshwe kwenye kituo chao cha afya.
Inadaiwa kuwa mkutano huo ulilenga kuzungumzia matumizi ya gari la kubebea wagonjwa lililotolewa msaada kwa kituo cha afya Mtowisa na mashirika ya Africare, Jhpego na Plan International kupitia mradi wanaotekeleza wa wazazi na mwana.
Mmoja wa wananchi hao, George Edwin alisema waliwakatalia madiwani hao wasifanye mkutano wa hadhara eneo hilo kwani haukuwa na tija kwao na walichokuwa wakikihitaji na kuona gari hilo la wagonjwa.
“Hawa jamaa wanaleta siasa kwenye mambo ya msingi, gari lilitolewa msaada kwa kituo cha afya Mtowisa, lakini linafanya shughuli nyingine mjini… hatujaliona kwa zaidi ya miezi miwili na nusu, wajawazito watatu wamekufa kwa kukosekana gari hilo, sasa wanakuja na siasa, sisi tumewaeleza mkutano haufanyiki ila tunataka gari lirudishwe kituoni,” alisema.
Alisema baadaye madiwani hao walielewa na kupiga simu ofisi ya mkurugenzi, ambapo aliamuru gari hilo lirejeshwe kituoni hapo na kupokelewa kwa shangwe na wananchi hao.
Edwin akizungumzia jaribio la kulichoma moto gari hilo, alisema zilikuwa hasira tu za vijana, lakini baadae walikaa na kutafakari kuona umuhimu wa gari hilo kurudi kituoni kuendelea kutumika kwa malengo yaliyokusudiwa na si kutumiwa na mkurugenzi kwa shughuli nyingine.
Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Edes Maembe alikiri wao kupata wakati mgumu baada ya kugomewa na wananchi hao, lakini alisisitiza kwamba mkutano huo ulilenga kueleza hatua ambazo madiwani wamepanga kuchukua baada ya uchunguzi kukamilika kuhusu tuhuma zisizo sahihi za gari hilo kwani sehemu kubwa lilikuwa likionekana wilayani Mpanda, Katavi.
Mwenyekiti Maembe aliongeza kuwa utaratibu uliowekwa hivi sasa ni kuhakikisha gari hilo linakaa muda wote kituoni hapo ili litumike kwa walengwa waliokusudiwa kwenye mradi huo ambao ni wakazi wa bonde la ziwa Rukwa na si vinginevyo.
Hivi karibuni kulitokea tafrani baada ya mjamzito kufariki dunia wakati akisubiri gari litoke mjini ili limpeleke hospitali ya mkoa mjini Sumbawanga kwa upasuaji baada kushindwa kujifungua kwa njia ya kawaida, lakini lilichelewa kwa zaidi ya saa saba hivyo wananchi kukasirika na kuvunja vioo vya gari huku likinusurika kuchomwa moto.
Chanzo:Tanzania daima
Jika Anda menyukai Artikel di blog ini, Silahkan klik disini untuk berlangganan gratis via email, dengan begitu Anda akan mendapat kiriman artikel setiap ada artikel yang terbit di Creating Website

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Rukwa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa