Home » » MAPYA YAIBUKA NDOA ILIYO VUNJWA NA MAHAKAMA

MAPYA YAIBUKA NDOA ILIYO VUNJWA NA MAHAKAMA


SAKATA la ndoa iliyovunjwa na Mahakama ya Mwanzo Wilaya ya Nkasi, Rukwa limeingia katika sura mpya baada ya kubainika kuwa mume aliyeomba kuvunjwa kwa ndoa yake, Ndebile Kazuri, alimkatisha masomo mkewe baada ya kumtia mimba akiwa darasa la sita.
Kwa mujibu wa vyanzo vya habari ambavyo mwandishi wa habari hii amevipata, Kazuri ambaye hivi karibuni ameiomba mahakama hiyo kuvunja ndoa yake na Maria Tarafa kwa madai ana kiburi na mdokozi wa vitu ndani ya nyumba yao, alimkatisha masomo na baadaye kumuoa mwaka 2004.
Taarifa zinaeleza kuwa Kazuri alikatisha masomo ya Maria akiwa Shule ya Msingi Isale wilayani Nkasi wakati huo akiwa na miaka 15 na alijifungua mtoto akiwa na miaka 16.
Ilidaiwa kwamba baada ya kupata ujauzito, wazazi wa pande zote mbili walizungumza kifamilia na kukubaliana wasimshtaki Kazuri kwa kuwa atafungwa jela huku Maria na mtoto wake watakosa huduma, hivyo walikubaliana waoane ndipo mwanaume huyo alipolipa mahari na kufunga ndoa.
Akizungumza na gazeti hili, Maria alikiri kukatishwa masomo na Kazuri mwaka 2003 akiwa darasa la sita, lakini kwa kuwa baba zao walikuwa marafiki walikubaliana waoane.
Alisema aliunganishwa na mumewe Kazuri mwaka 2004 akiwa na umri wa miaka 16 baada ya kulipa mahari  ya ng’ombe kwa familia yao.
“Inaniuma kwa kitendo ambacho ananifanyia kwa sasa kwani alinikatisha masomo, kanipotezea muda wangu na kaniongezea mzigo wa watoto wanne na anataka niende kuishi nao peke yangu baada ya kwenda kuongopa mahakamani,” alisema Maria.
Alisema sababu alizozitoa mahakamani si za kweli kwani amekuwa akimpiga na kumnyanyasa ndani ya ndoa yake na kumtaka aondoke kwake na kwenda kuishi kwao.
Maria alisema kuna kipindi mtalaka wake huyo aliwahi kumfukuza akiwa na watoto wawili na kurudi nyumbani kwao, lakini baadaye alikuja kuomba radhi na kutaka apewe mke wake aende kuishi naye.
Kazuri alifungua kesi namba katika Mahakama ya Mwanzo, Namanyere Oktoba 28, 2013 iliyosikilizwa na Hakimu B. Stanley na Novemba 18, 2013 hakimu huyo aliamuru ndoa ivunjwe.
Mahakama ilivunja ndoa hiyo na kuamuru Maria aondoke na watoto wawili kati ya wanne aliozaa na mumewe bila kueleza namna watakavyopata huduma toka kwa baba yao.
Katika hukumu yake, mahakama iliamuru watoto wa miaka saba na tisa watabaki kwa baba yao na wenye miaka chini ya saba kubaki na mama yao.
Mahakama hiyo ya mwanzo pia iliamuru mke apewe magunia tisa ya mahindi kati ya 10 ambayo walizalisha wote na mabati saba yaliyokuwa nyumbani kwao.
Hata hivyo, alipotafutwa Kazuri kuzungumzia madai hayo kwa njia ya simu hakuweza kupatikana kwani taarifa ambazo zimetufikia ni kwamba, kwa sasa anashikiliwa na Jeshi la Polisi Wilaya ya Nkasi kwa kitendo cha kuvunja nyumba ya mtalaka wake na kumtishia kumdhuru huku akimtaka aondoke kwake.
Chanzo;Tanzania Daima
Jika Anda menyukai Artikel di blog ini, Silahkan klik disini untuk berlangganan gratis via email, dengan begitu Anda akan mendapat kiriman artikel setiap ada artikel yang terbit di Creating Website

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Rukwa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa