Mussa Mwangoka, Sumbawanga. Rukwa yetu
WAKAZI wa mkoa wa Rukwa wametakiwa kuweka akiba ya chakula cha kutosha kwa kuwa upo uwezekano mkubwa wa baadhi ya maeneo ya mkoa huo kukabiliwa na baa la njaa kutokana na kupungua kwa uzalishaji wa mazao unaosababishwa na mabadiliko ya tabia nchi.
Mratibu wa asasi isiyo ya kiserikali inayojishughulisha na utunzaji wa mazingira ya Kaengesa Environmental Conservation Society (Kaeso) iliyopo wilaya ya Sumbawanga, Joel Amon, alitoa tahadhari hiyo jana wakati akizungumza na mwandishi wa habari ofisi kwake kuhusu athari zilizojitokeza kutokana na mabadiliko ya tabia nchi.
Alisema kuwa hali ya uzalishaji wa mazao ya chakula hususani mahindi katika Wilaya za Sumbawanga na Nkasi si wakuridhisha ukilinganisha na misimu mingine ya kilimo hali iliyojitokeza kutokana na mabadiliko ya tabia nchi yaliyosababishwa na uharibifu wa mazingira.
"Katika maeneo mengi ya mkoa huu kumejitokeza ukame kwa kuwa mvua hazijanyesha lakini yale ambayo mvua zimenyesha si kwa kipindi ambacho wakulima walitegemea, kuna sehemu mvua ziliwahi isivyo kawaida na zikakatika mapema sana...... sasa hii iliathiri kwa namna moja au nyingine” alisema.
Pia alisema kuwa tatizo jingine lililosababisha kuwepo kwa hali hiyo ni uchakachuaji na udanganyifu mkubwa uliojitokeza katika zoezi la usambazaji wa pembejeo za kilimo kupitia mfumo wa vocha.
Alisema kuwa ni vizuri wakulima wakaweka akiba ya chakula badala ya kuuza chote kama ilivyo kawaida yao na kwamba pamoja na uzalishaji wa chakula kuwa wa chini ukilinganisha na msimu mingine, pia mavuno yanatarajia kuwa kidogo na hali itakuwa mbaya miezi michache ijayo.
Kwa mujibu wa takwimu za kilimo, zinaonyesha kuwa kwa msimu wa kilimo wa 2010 hadi 2011 ulizalisha ulikuwa tani 2,136,345 za mazao ya chakula huku msimu ujao wa mavuno wanategemea kuvuna 2,518,270 za mazao cha chakula ambazo huenda zisifikiwe.
0 comments:
Post a Comment