Imeandikwa na Peti Siyame, Nkasi
MWANAMKE mkazi wa Kijiji cha China Kata ya Kate, Nkasi, Rukwa,
Telestina Silanda (45) ameuawa kwa kuchinjwa na mwili kucharangwa na
watu wasiojulikana akiwa amelala nyumbani kwake usiku wa kuamkia jana.
Ndugu wa marehemu, Charles Silanda alidai tukio hilo lilitokea saa
mbili usiku watu wasiojulikana waliovalia “kininja” walipovamia nyumba
yake (shangazi) na kumshambulia kwa panga na kumchinja.
Alisema hadi wao wanajulishwa tukio hilo na kukimbilia eneo la tukio
walikuta shangazi ameuawa na wauaji hao wametoweka katika eneo la tukio.
Ofisa Mtendaji wa kijiji hicho, Konrad Kauzeni alisema mwanamke huyo
aliuawa kinyama, kwa kukatwa miguu yake yote miwili na kuitenganisha na
mwili, kichwa na shingo.
Alisema mume wa mwanamke huyo alikuwa amekwenda porini kurina asali
kwenye mizinga yake na aliporejea nyumbani alikuta mkewe kauawa kikatili
na waliofanya tukio hilo hawajafahamika.
Mkuu wa Wilaya ya Nkasi, Said Mtanda ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati
ya Ulinzi na Usalama amethibitisha kutokea kwa mauaji hayo akisema
ataenda kijiji hicho wananchi wapige kura za maoni ili kuwabaini wauaji
hao.
Alisema ni jambo lisilokubalika watu kufanya uhalifu mkubwa kiasi
hicho na wakaachwa, hivyo kura za maoni zitasaidia kuwanasa wauaji hao
ili sheria ichukue mkondo wake. Aliwataka wakazi wa eneo hilo kwenda
ofisini kwake kutoa taarifa za siri kwa wale wanaowafahamu.
CHANZO HABARI LEO
0 comments:
Post a Comment