Walter Mguluchuma Na Arine Temu .
Nkasi Rukwa yetu Blog
SERIKALI
wilayani Nkasi mkoani Rukwa imewaonya walimu wa shule za msingi na
sekondari wilayani humo kuacha tabia ya kujihusisha na mahusiano ya
kimapenzi na wanafunzi wao.
Mkuu wa wilaya hiyo Said Mtanda alitoa onyo hilo kwa
walimu hao jana wakati akizungumza katika kikao cha kazi huku
akiwatuhumu baadhi ya walimu kujihusisha na mahusiano ya kimapenzi na
wanafunzi wao.
Alisema kuwa miongoni mwa mambo ambayo yanamuudhi yeye
akiwa ni mkuu wa wilaya hiyo ni tabia ya walimu kuwa na mahusiano ya
kimapenzi na wanafunzi kwani tabia hizo zinawahairibia wanafunzi hao
ndoto zao za baadae.
"Ole wake mwalimu yeyote atakayebainika kuwa na
mahusiano ya kimapenzi na mwanafunzi,serikali ya wilaya itahakikisha
mwalimu huyo anachukuliwa hatua kari kwani hatupo tayari kuwaendekeza
walimu wa aina hii katika wilaya ya Nkasi"..alisema
Aliwaonya pia wanaume wote wilayani humo kuacha tabia ya
kuwalaghai wanafunzi na kuwa na mahusiano nao ya kimapenzi kwani ni
tabia mbaya na yeye ataongoza vita ya kupambana na wanaume wote wenye
tabia hiyo.
Aidha Mtanda aliwataka walimu wilayani humo kuongeza
bidii katika suala la kufundisha kwani anataka wilaya hiyo ifanye vizuri
kitaifa kwakuwa inawalimu waliosoma katika vyuo ambavyo walimu wa mikoa
mingine inayoongoza wamesoma sasa kwanini wilaya ya Nkasi isiongoze
kitaifa.
Naye mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Nkasi Julius
Kaondo aliwataka watendaji wilayani humo kujituma katika kufanya kazi
hususani katika suala zima la kukusanya mapato ambayo yanaiwezesha
serikali kuwahudumia wananchi.
Alisema kuwa kila mtendaji ahakikishe kuwa mapato ya
serikali yanaifikia serikali kwani sasa hivi serikali ya awamu ya tano
imeamua kuwatumikia wananchi kwa dhati hivyo wasiwepo wajanja wachache
ambao wataiangusha serikali kwani kila mwananchi anahaki ya kufaidi
ukwasi wa halmashauri ya Nkasi na taifa kwa ujumla.
Alisema kuwa serikali hivi sasa inaboresha ujenzi wa
barabara, afya,maji elimu na maeneo mengine itaweza kufikia malengo yake
iwapo wananchi watalipa mapato na watendaji watayakusanya na
kuhakikisha yanaifikia serikali na hatimaye kuwanufaisha wananchi wote.
0 comments:
Post a Comment