Kaimu Mkurugenzi wa Lishe wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk Vincent Assey
LICHA ya mkoa wa Rukwa kuwa miongoni mwa mikoa inayolima chakula kwa
wingi nchini, unaongoza kwa udumavu, ukiwa na asilimia 56.6 ya watoto
wenye tatizo hilo.
Takwimu hizo za mwaka jana zilitolewa juzi na Kaimu Mkurugenzi wa
Lishe wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk
Vincent Assey wakati wa uzinduzi wa ripoti ya lishe ya dunia
iliyozinduliwa na Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan.
Mikoa mingine inayofuata kwa tatizo hilo linalotokana na lishe duni
ni Ruvuma yenye asilimia 44.4, Kagera asilimia 41.7 na Iringa asilimia
41.6.
Kwa mujibu wa takwimu hizo, mwaka 2010, Rukwa ilikuwa na udumavu wa
asilimia 50 na hivyo hali imezidi kuwa mbaya badala ya kuimarika. Mwaka
huo (2010) Ruvuma ilikuwa na asilimia 46, Kagera asilimia 44 na Iringa
asilimia 52.
Kwa mujibu wa takwimu hizo, mikoa ambayo ina afadhali kuhusu tatizo
la udumavu ni Dar es Salaam yenye asilimia 14.4, Shinyanga yenye
asilimia 27.7, Tabora yenye asilimia 27.9, Kilimanjaro yenye asilimia 29
na Singida yenye asilimia 29.2.
Wastani wa takwimu za kitaifa za mwaka jana ni asilimia 34 kutoka asilimia 42 mwaka 2010.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi Jukwaa la Lishe Tanzania (Panita), Dk
Tumaini Mikindo, alisema udumavu ni hali ya akili na mwili wa mtoto
kutokukua kwa kiwango kinachotakiwa kutokana na lishe duni na mara
nyingi hutokea katika kipindi cha siku 1,000 zinazohesabiwa tangu mimba
kutungwa hadi mtoto anapofikisha umri wa miaka miwili.
Chanzo Na Habari Leo
0 comments:
Post a Comment