Home » » RIPOTI:WATOTO 863 HUFANYIWA UKATILI KILA MWAKA

RIPOTI:WATOTO 863 HUFANYIWA UKATILI KILA MWAKA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Mmoja kati ya watoto watatu wa kike hufanyiwa ukatili kabla ya kufikisha miaka 18  

Wengi hukaa kimya bila kutoa taarifa pale wanapokutana na kadhia licha ya kwamba wananyanyaswa na kutumikishwa na watu wao wa karibu, wanaowaamini na kuwategemea.
Siyo kwa sababu  hawaumii au kuathirika, bali ni kutokana na woga wa yale watakayokumbana nayo baada ya ‘kuchoma utambi’ kwa vyombo vya usalama, ili kupata msaada zaidi.
Licha ya hao wanaojitambua,  kuna kundi la wale wasiojua kinachoendelea duniani, ambao hujikuta wakiishia katika madampo kwa sababu tu wazazi wao walishindwa kuwalea baada ya kupata mimba katika mazingira tatanishi.
Hii ndiyo hali halisi wanayokumbana nayo watoto wa sehemu mbalimbali nchini katika maisha yao ya kila siku, ya kufanyiwa vitendo vya kikatili.  Jamii hiyo imejikuta ikiwa pweke na isiyo na matumaini ya furaha.
Kwa mujibu wa Ripoti ya Haki za Binadamu ya mwaka 2013 iliyotolewa na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) hivi karibuni, anasema matukio ya unyanyasaji kwa watoto yameongezeka nchini licha ya jitihada lukuki za kupambana nayo.
Ripoti hiyo inabainisha kuwa kuna kesi 863 za watoto kulawitiwa na ndugu wa karibu wakiwamo baba, kaka, binamu na wajomba.
Mbali na hao waliolawitiwa, ripoti hiyo inaongeza kuwa wapo watoto zaidi ya 250 ambao walitupwa au kutelekezwa na walezi au wazazi wao.
“Vitendo vya utelekezaji watoto vimekuwa vikiripotiwa kutoka katika hospitali na vituo ya afya. Watoto wachanga huachwa na mama zao saa chache baada ya kuzaliwa,” inasema sehemu ya taarifa hiyo.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo ya 11 tangu zilipoanza kutolewa mwaka 2002, wazazi wa watoto hao hufanya vitendo hivyo kwa madai ya kutokuwa tayari kulea viumbe hivyo, kutokana na ugumu wa maisha.
Kutokana na kushamiri vitendo hivyo, mkurugenzi mtendaji wa kituo hicho, Dk Hellen Kijo-Bisimba anapendekeza kuanzishwa kwa vituo vitakavyotoa elimu ya malezi kwa wazazi na walezi, ili kupunguza ukatili kwa watoto.
Hatua hiyo pia inaungwa mkono na Sia Malamsha, mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agustino, ambaye anasema wasichana wengi hujikuta wanapata mimba wakati hawajajiandaa kuwa mama, hivyo hutafuta njia ya kukwepa majukumu.
“Unajua wengi huwa hawapo tayari kubeba majukumu ya ulezi, hivyo huishia kumtupa au kumtelekeza mara tu baada ya kujifungua,” anabainisha Sia anayesomea sheria.
Anaongeza kuwa tatizo hilo linaweza kuepukika iwapo serikali na wadau wengine watafanya jitihada za kutoa elimu ya afya ya uzazi bila kuchoka, ili wazazi wafahamu taratibu za kujiandaa kabla kupata ujauzito.
Hata hivyo, binti huyo anatoa njia mbadala ambayo inaweza pia kupunguza idadi ya watoto waliotelekezwa mitaani akisema ni kuasili.
Sia anasema kuwa serikali ijaribu kupitia upya sheria zake na kuzifanyia mabadiliko kwa ajili ya kurahisisha watu wanaotaka kuasili watoto, waweze kuwapata kirahisi bila usumbufu.
Mbali na kurahisisha taratibu za kuasili, pia anaongeza kuwa elimu itolewe kwa jamii kujua namna ya kuasili watoto na taarifa zinazohusu masuala hayo ziwe wazi.
“Unajua kuna watu hawana watoto na wana shida ya kupata watoto wa kuasili ili kuziba pengo walilonalo. Lakini wanashindwa kujua watapata wapi watoto kutokana na kukosa taarifa sahihi juu ya namna ya kuwapata na namna ya kuwaomba,” anasema Sia.
Ripoti hiyo pia inasema kuna kesi nyingi  za vipigo kwa watoto, ukilinganisha na aina nyingine ya unyanyasaji ambao iliripotiwa mwaka jana kutoka katika shule na ndani ya familia mbalimbali.
Inabainisha kuwa baadhi ya kauli za viongozi pia zilichochea unyanyasaji wa watoto, ikiwemo ile ya aliyekuwa naibu waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Phillipo Mlugo ya kutangaza kuwa serikali ina mpango wa kurudisha viboko shuleni kama njia ya kuhamasisha uelewa kwa wanafunzi.
Msemaji wa Jeshi la Polisi nchini, Advera Senso anasema matukio mengi ya unyanyasaji watoto hayaripotiwi katika vyombo husika kwa ajili ya hatua zaidi, kutokana na watu wengi kuyapuuza kuwa siyo uvunjifu wa haki za watoto.
Senso anaunga mkono ripoti ya LHRC na kuongeza kuwa, wazazi na walezi wengi ndio wamekuwa mstari wa mbele kutekeleza matukio hayo kutokana na ulevi au ushirikina.
Anaongeza kuwa ili kukabiliana na hali hiyo, Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na wadau wengine, lilianzisha madawati maalumu ya kushughulikia matukio yote ya unyanyasaji kwa wanawake na watoto katika mikoa yote nchini.
“Tangu tulipoanzisha madawati hayo idadi ya watu wanaoripoti uvunjifu wa haki za watoto imeongezeka ukilinganisha na kipindi cha nyuma,” anasema.
Hapo awali, kulikuwa na makabila mengi ambayo yalikuwa hayajui vitendo wanavyofanya kuwa ni ukatili kwa wanawake na watoto,” anasema Senso akiongeza kuwa mafanikio hayo ni matokeo ya ushirikiano na wadau kama Wizara ya Jinsia, Wanawake na Watoto na taasisi za kijami (NGOs).
Anabainisha kuwa kwa sasa wana utaratibu wa kuwahoji faragha watoto, na kwamba hutoa siri nyingi juu ya ukatili unaofanywa dhidi yao.
“Tunaendelea kufanya maboresho ya vituo vya kufanyia mahojiano katika vituo vya polisi mbalimbali nchini ili kuhakikisha tunapunguza vitendo hivi. Lazima watu wajue kuwa awe mzazi au mlezi; tukimkamata tutamfikisha mahakamani,” anaonya Senso.
Matokeo ya ripoti ya LHRC yameendeleza tu takwimu za utafiti wa awali uliofanywa na Wizara ya Maendeleo ya Wanawake, Jinsia na Watoto kwa kushirikiana na Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulia watoto (UNICEF) na  Kituo cha Kudhibiti Magonjwa (CDC).
Iliongeza kuwa watoto wengi hapa nchini walifanyiwa ukatili wa kingono, kimwili na kunyanyaswa kisaikolojia kabla ya kufikisha miaka 18. Zaidi ya asilimia 70 ya watoto wote walifanyiwa ukatili wa kimwili na kisaikolojia.
Hata wakati ukatili kwa watoto ukiendelea, serikali nayo imekuwa ikifanya jitihada kupambana wa suala hilo, ikiwemo kuwatoa watoto katika mazingira magumu.
Katika hotuba yake ya bajeti ya mwaka wa fedha unaoishia, Waziri wa Maendeleo ya Wanawake, Jinsia na Watoto, Sophia Simba alisema Serikali iliwatambua watoto  849,051 wakiwemo wasichana 407,544 sawa na asilimia 48 na wavulana 441,507 sawa na asilimia 52.
“Watoto hao kwa sasa wanapatiwa huduma za elimu, afya, chakula na msaada wa kisheria na kisaikolojia kupitia wadau mbalimbali,” alisema Simba akionyesha mafanikio ya mwaka 2012/13.
Pia serikali kwa kushirikiana na wadau waliandaa mpangokazi wa miaka mitatu (2013–2016) wa kutokomeza ukatili kwa watoto, uliozinduliwa mwaka jana.
Pamoja na jitihada hizo za serikali na wadau, bado umma una wajibu wa kuhakikisha unalinda haki za watoto kwa kusimamia kikamilifu Sheria ya Mtoto namba 21 ya mwaka 2009 na sera yake ya mwaka 2008.
Chanzo;Mwananchi
Jika Anda menyukai Artikel di blog ini, Silahkan klik disini untuk berlangganan gratis via email, dengan begitu Anda akan mendapat kiriman artikel setiap ada artikel yang terbit di Creating Website

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Rukwa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa