Home » » Elimu ya kutunza mazingira yaokoa maliasili Rukwa

Elimu ya kutunza mazingira yaokoa maliasili Rukwa


KULINDWA kwa vyanzo vya maji na misitu ya asili katika maeneo mbalimbali ya kata ya Sintali wilayani Nkasi mkoani Rukwa kumetajwa kuwa sehemu ya matokeo chanya ya elimu ya utunzaji mazingira iliyotolewa mwanzoni mwa mwaka huu kwa wakazi wa kata hiyo.
Mtandao wa asasi zisizo za kiserikali wilayani Nkasi (Nkango) ndiyo ulitoa elimu hiyo kupitia mdahalo uliofanyika kijijini Sintali kwa ufadhili wa The Foundation for Civil Society. Viongozi na wakazi wa kata hiyo wanakiri kuwa elimu waliyoipata kupitia mdahalo huo miezi kadhaa iliyopita imekuwa na manufaa makubwa kwani imewaongezea uelewa kwenye masuala ya utunzaji wa mazingira na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.
Kaimu ofisa mtendaji wa kata ya Sintali, Halle Siame, anasema baada ya kupata elimu serikali za vijiji vya katahizo zimekuwa na mikakati endelevu ya kutunza mazingira ikiwemo kuweka doria za kushtukiza kwenye maeneo ya misitu ya asili kwa ajili ya kuwabaini watu wanaokata miti hovyo na kuingiza mifugo kiholela kwenye misitu hiyo.
“Kwa kata hii tuna vijiji vya Sintali, Nkana, Mkomanchindo na Kasapa na hivi vyote vimekuwa na mikakati ya kuhakikisha misitu ya asili iliyotengwa inalindwa. Uongozi wa kijiji husika unaweza kufanya doria ya mara kwa mara kwenye misitu na kubaini waharibifu wa misitu hiyo,” anasema Halle Siame.
“Lakini pia kumekuwa na hamasa kubwa ya taasisi mbalimbali kujishughulisha na uoteshaji wa miche ya miti kwa ajili ya kuigawa kwa wananchi tayari kwa kuipanda kwenye maeneo yao. Lakini pia utaona kasi ya kuchoma mapori yetu imepungua ikilinganishwa na awali. Viongozi wa vijiji pia mara kwa mara wanaandaa mikutano ambayo wanaitumia kutoa elimu juu ya utunzaji wa mazingira,” ameongeza Siame.
“Ni dhahiri kuwa wakazi wengi sasa katika kata yetu wametambua umuhimu wa kuyatunza mazingira. Wametambua pia juu ya athari zinazoikumba dunia kutokana na kuharibiwa kwa mazingira kwa kuwa tayari zimetukumba hata sisi. Moja kati ya athari hizo ni kutokuwa na misimu ya mvua inayoeleweka kama ilivyokuwa miaka ya nyuma,” anasema kaimu ofisa mtendaji wa kata hiyo.
Anasema wanaokamatwa na kubainika wanakata miti hovyo na kuchoma mkaa bila kuwa na kibali wanaadhibiwa sawa na wanaochoma moto mapori ambapo hutakiwa kulipa faini ya kati ya Sh 20,000 hadi Sh 50,000. Naye Ofisa Mtendaji wa kijiji cha Sintali, Crisense Silanga, anasema kwa kijijini hapo kamati ya huduma za jamii ndiyo yenye jukumu la kutembelea msitu wa asili uliopo kilomita chache kutoka eneo la makazi ya kijiji hicho.
Kwa mujibu wa Silanga utendaji wa kamati hiyo kwenye kuilinda misitu na vyanzo vya maji vilivyopo kijijini hapo umekuwa na ufanisi mkubwa katika siku za hivi karibuni. Anasema bila shaka ni kutokana na wakazi kuanza kupata uelewa juu ya nini madhumuni ya vijiji kulinda rasilimali hizo muhimu kwa kizazi kilichopo na kijacho.
“Ukiangalia ugumu uliokuwa ukizikumba kamati hizi kwa miaka ya nyuma zilizopotembelea msitu na vyanzo vya maji ni tofauti na sasa. Kumekuwa na ushirikiano mkubwa wa wananchi. Wapo baadhi ya wananchi wanaothubutu hata kutoa taarifa pale wanapoona mtu akifanya uharibifu kwenye vyanzo vya maji au akikata miti kwenye msitu wa kijiji,” amesema Crisense Silanga.
“Zamani haikuwa hivyo. Hata tulipochukua hatua dhidi ya wahusika wapo wananchi walioonekana kutulaumu na kujenga chuki kwa wajumbe wa kamati na uongozi wa kijiji kwa ujumla. Wao walijua ni uonezi na kila mtu ana haki ya kuingia kwenye misitu tuliyotenga na kufanya kile atakacho hata bila kibali,” amefafanua Silanga.
Alisema pia kwa sasa zoezi la kupunguza mifugo ili iendane na eneo lililotengwa kwa ajili ya malisho ya mifugo halisumbui sana. Wakazi ambao miaka ya nyuma walikuwa wakiwapokea kiholela wafugaji na kuwapa hifadhi sasa ni wachache waanaoendelea na tabia hiyo. Lakini pia wafugaji wanakubali kuhamisha mifugo yao kupunguza idadi ambayo awali ulikuwa mzigo mkubwa kwa kijiji.
Hata hivyo, mwalimu mkuu wa shule ya msingi Sintali, Sezari Katelema, anasema elimu zaidi bado inahitajika. Anasema bado wapo wakazi katika kijiji hicho wanaopingana na mikakati inayofanywa na wadau wa utunzaaji wa mazingira. “Wapo wafugaji ambao hawataki kuona miti ikipandwa wakiamini watakosa maeneo ya kulishia mifugo yao.
Unapopanda wao hung’oa miche hiyo. Mfano mzuri ni miti tuliyopanda katika eneo moja la shule, kuna watu walipita usiku na kuing’oa. Wanataka maeneo yawe wazi ili mifugo yao izurure hovyo. Nadhani elimu bado inahitajika zaidi, hatuwezi kubadilika wote kwa pamoja,” amesema Sezari Katelema akiwa ofisini kwake.
Mwalimu Katelema anakitaja kijiji cha Sintali kuwa kati ya vijiji vilivyovyo na bahati kubwa ya kuwa na vyanzo vya maji vya asili vingi. Mfano ni kile kilichopo jirani na shule ambacho hutiririsha maji kwa mwaka mzima.
“Kijiji hiki kinaweza kuongoza kwa mkoa mzima wa Rukwa kwa kuwa na maji mengi. Serikali na wadau wanapaswa kuwekeza huku kwa kuhakikisha wanashirikiana na wananchi kuweka mikakati madhubuti ya kuvilinda vyanzo hivi ili viwe endelevu. Naamini uelewa mdogo huu uliopo si tatizo la wanakijiji, tatizo ni wasimamizi hawajatoa elimu ya kutosha,” anaongeza Katelema.
Chanzo;Habari Leo
Jika Anda menyukai Artikel di blog ini, Silahkan klik disini untuk berlangganan gratis via email, dengan begitu Anda akan mendapat kiriman artikel setiap ada artikel yang terbit di Creating Website

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Rukwa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa