WAKATI majeshi mengine yakijiimarisha kijasiri na ukakamavu kwa
kufanya mazoezi ya mwili kwa vifaa bora, askari wa jadi, maarufu
sungusungu ambao ni vijana wa kiume wapatao kiume 83 wamelazimika
kuchanjwa chale mwili mzima kuongezewa ujasiri.
Vijana hao walichanjwa chale na waganga wa kienyeji ili wawe wakali
pia wawe jasiri wanapokabiliana na wahalifu hata kama wahalifu wana
silaha nzito.
Sherehe ya kuchanjwa ilihusisha sungusungu wa vijiji vya Mwale na
Ng’ongo vilivyopo katika Bonde la Ziwa Rukwa katika wilaya ya
Sumbawanga, Rukwa, ambako mbuzi wawili walichinjwa kwa ajili ya kitoweo
cha askari hao. Walikula kwa ugali wa dona.
Gazeti hili lilifika uwanja uliotumika kwa sherehe hizo ndani ya
msitu huo na kushuhudia askari hao vijana wenye umri kati ya miaka 20 na
40 wakichanjwa chale mwili mzima na waganga wanne wa kienyeji
waliokodishwa kuifanya kazi hiyo .
Wakizungumza na gazeti hili kwa masharti ya kutoandikwa majina yao
gazetini, vijana wengine wa miraba minne walidai kuwa na imani ya dawa
hizo za kienyeji kuwa zina uwezo wa kuwafanya kuwa wakali na jasiri
zaidi.
“Tukishapigwa chale mwili mzima basi tutakuwa na uwezo wa kubaini
mhalifu kabla hata hajafanya uhalifu hivyo tutaweza kuzuia uhalifu kabla
haujafanyika. Isitoshe tutakuwa jasiri kupita kiasi, nguvu za kupita
kiasi na hatutaogopa kukabiliana na mwalifu hata kama atakuwa na silaha
nzito,” alisisitiza mmoja wao .
Akizungumza na gazeti hili Kamanda wa Jeshi hilo la Sungusungu,
Mahona Boniface alisema kupigwa chale kwa askari hao vijana wa
sungusungu ni agizo la mtemi wao wa sungusungu aitwae Clement Mbogatabu
alilolitoa mara baada ya kuchaguliwa kushika nafasi hiyo katika uchaguzi
uliofanyika hivi karibuni.
“Mie ndiye niliyepiga mbiu kuwakusanya askari hawa na kuwapatia
maagizo ya mtemi wetu wa sungusungu wote waliafiki na leo (juzi)
tumekusanyika kwenye uwanja huu ambapo kila askari ameagizwa aje na
wembe wake mwenyewe mpya na kiasi cha Sh 500 ikiwa ni ujira wa mganga
atakaye mchanja chale,” alisema Mbogatabu.
Waganga hao wa kienyeji waliokodiwa kuifanya kazi hiyo walitajwa kuwa
ni Juma Aron, Shinje Buzuka na Lutema Mugesa huku jina la mganga wa nne
halikuweza kupatikana.
Alisema waganga hao wanatoka kijiji cha Uzia na mwingine ni mkazi wa
kijiji cha Santaukiwa vilivyopo katika Bonde la Ziwa Rukwa wilayani
Sumbawanga ambapo shughuli hiyo walifanya juzi kuanzia saa tatu asubuhi
hadi saa nane mchana .
Walisema baada ya kuchanjwa askari hao vijana wa kiume wa sungusungu
wamezuiwa kukutana kimwili na mwanamke hata kama wameoa kwa muda wa siku
tatu baada a kupita siku hizo watakusanyika tena ambapo wataogeshwa
dawa ndipo wataruhusiwa kufanya tendo la ndoa.
CHANZO GAZETI LA HABARI LEO
0 comments:
Post a Comment