Home » » MAHAKAMA YALAAMIKIWA KUVUNJA NDOA

MAHAKAMA YALAAMIKIWA KUVUNJA NDOA

MAHAKAMA ya Mwanzo Namanyere, wilayani Nkasi, imelalamikiwa kuvunja ndoa iliyokuwa na mgogoro bila kugawanya mali iliyochumwa na wanandoa wakiwa pamoja.
Maria Tarafa (25), mkazi wa Kijiji cha Isale ambaye ni mmoja wa wanandoa hao, alitoa malalamiko hayo mjini hapa alipozungumza na mwandishi wa habari hizi, huku akiituhumu mahakama kutompa nafasi ya kujitetea.
Alisema mumewe, Ndebile Kazuri (31) alikuwa akitaka kumtelekeza yeye na watoto wao wanne kwa muda mrefu kwa kutaka kuivunja ndoa kinyemela, lakini alikuwa akimshinda kila alipoitisha vikao vya wazazi na viongozi wa vijiji na kata akitaka kuivunja ndoa hiyo bila kutoa haki kwake na watoto.
Maria alisema mume huyo ameishi naye tangu mwaka 2003 na kufanikiwa kupata watoto wanne ambao alikuwa akiishi nao, huku mzazi mwenzie huyo akiishi na mwanamke mwingine eneo hilo ambaye pia amezaa naye.
“Licha ya kuishi naye, amekuwa akinipiga na kunifukuza niondoke kwake na watoto wangu nirudi kwetu, lakini mimi nimekataa mara zote na kumwambia nitakuwa tayari kuondoka baada ya kupata haki zangu na watoto,” alisema.
Alisema mumewe aliamua kwenda baraza la kata na kuomba barua ili aende mahakamani kuiomba ivunje ndoa hiyo. Kazuri alifungua kesi hiyo namba 26/2013 Oktoba 28 mwaka jana.
Alisema mahakama ilimwita kwa mara ya kwanza na kumsomea maelezo ya mdai (mumewe) ya kuomba ndoa yao ivunjwe, lakini yeye alipinga na kutaka awasilishe maelezo yake, lakini iligoma kwa madai ilichohitaji kwa mlalamikiwa ni kujibu kama yupo tayari au la.
“Niliomba nipewe nafasi ya kuzungumza upande wangu, lakini walikataa na kuniambia wamekuja kusikiliza kesi ya talaka na si maelezo mengine,” alisema.
Alieleza Novemba 18 mwaka jana baada ya kukiri kuwa yupo tayari kuachana na mumewe iwapo atapata haki zake na watoto, mahakama ilivunja ndoa hiyo na kuamuru aondoke na watoto wawili bila kueleza namna watakavyopata huduma toka kwa baba yao.
Alisema mahakama iliamuru watoto wa miaka 7 na 9 watabaki kwa baba yao na yeye kuondoka na wawili wenye miaka chini ya saba.
Aliongeza kuwa mahakama iliamuru apewe magunia 9 ya mahindi kati ya 10 ambayo walilima pamoja na bati saba.
Akizungumzia sakata hilo, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya, Ramadhan Rugemalira, alisema mama huyo ana haki ya kufungua kesi ya madai kuomba mgawanyo wa mali na matunzo kwa watoto endapo hakuridhika na hukumu iliyotolewa.
Hata hivyo, Hakimu Rugemalira alisema huenda mtoa hukumu wa mwanzo aliteleza kwa kitendo cha kutoainisha namna watoto wanaobaki kwa mama watalelewa vipi.
Kazuri alipoulizwa juu ya mali ambazo mke wake anazilalamikia, yaani ng’ombe 127, nyumba mbili, mbuzi 30 na ardhi hekari 70, alisema mali hizo alipewa na baba yake wakati anaanza maisha.
Uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa habari hizi umebaini baba yake Kazuri (yaani Kazuri Moshi) ni marehemu, alifariki tangu Machi 2004 na mali zake kugawiwa kwa watoto wake.
Chanzo:Tanzania Daaima
Jika Anda menyukai Artikel di blog ini, Silahkan klik disini untuk berlangganan gratis via email, dengan begitu Anda akan mendapat kiriman artikel setiap ada artikel yang terbit di Creating Website

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Rukwa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa