Kauli ya Chikawe ni udikteta, aibu kwa demokrasia
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mathias Chikawe.
Wakizungumza na NIPASHE katika maeneo mbalimbali nchini jana, wadau
hao walidai kuwa, kufanya hivyo ni kusababisha vurugu na udikteta
mkubwa kwa nchi inayoendeshwa kwa misingi ya utawala bora na demokrasia.
Makamu wa Rais wa Baraza la Maaskofu Tanzania (Tec) na Askofu wa
Jimbo la Rulenge, mkoani Kagera, Severin Niwemugizi, alisema amelipokea
tamko hilo kama matamshi ya watu ambao hawajakomaa kisiasa, wasio
tayari kupokea maoni ya wengine tofauti na yao na kwamba halina haki
bali limejaa woga.
“Katika nchi ya demokrasia yenye viongozi wa namna hii hawana
tofauti na madikteta, ukianza kutishia wenzako kuwa ukisema maneno
nisiyoyapenda nakufuta huo ni udikteta,” alisema na kuongeza:
“Sheria ya kura ya maoni inasema kutakuwa na makundi ya ndiyo na
hapana, najiuliza ni kundi lipi la pande hizo, kwanini wawepo wanaozuiwa
wasihamasishe watu kusema hapana kama taasisi za serikali
zinazoruhusiwa kuhamasisha ndiyo?” alihoji.
ARUSHA: NI UDIKTETA
Baadhi ya asasi za kijamii na watu binafsi mkoani Arusha, walisema
tishio hilo ni udikteta ambao ni aibu kutolewa na viongozi katika nchi
inayothamini demokrasia na kwamba inapaswa kukemewa kwa vile ina lengo
la kupora uhuru wa kujieleza ambao upo kikatiba.
Mkurugenzi wa Shirika lisilo la kiserikali la Utetezi wa Haki za
Wafugaji, Warina Asali na Waokota Matunda (Pingo’s Forum), Edward
Porokwa, alisema kauli ya Waziri Chikawe ni tishio kubwa linalowanyima
uhuru wa kujieleza.
“Kweli kauli hii ni tishio kubwa na tunapaswa kuikemea, sababu
inatunyima haki na uhuru wa kujieleza kwenye masuala yetu yanayotuhusu
kama katiba pendekezwa,” alisema.
Mkurugenzi wa asasi ya Grassroot Youth Development Organisation
(GYDO), Henry Cigwasi, alishauri matamko mengine ya viongozi wa serikali
yatolewe baada ya kufanyiwa utafiti.
Alisema maisha yote ya binadamu ni siasa, kila kitu anachofanya ni
siasa, hivyo hawawezi kuacha kuzungumzia au kutoa elimu ya uraia bila
kuzungumzia masuala muhimu yanayohusu maisha yao.
Alisema huku akitoa mfano wa Katiba Inayopendekezwa, kuwa wapo
viongozi serikalini ambao wamesikika mara kadhaa wakiwahamasisha
wananchi kuipigia kura za ndiyo siku ya kupiga kura ya maoni
itakapowadia.
Lakini alisema wapo watu ambao wameichambua Katiba hiyo na kutoa
maoni tofauti na viongozi wa serikali, lakini kwa kuwa maoni yao
yanakinzana na viongozi wa serikali, wananyamazishwa.
“Kama kuna asasi au taasisi ya dini inatoa elimu kuonya kuhusu ubaya wa kitu fulani, tatizo lipo wapi hapo,” alisema.
Alishauri viongozi wa serikali kabla ya kutoa matamko kuhusu jambo
fulani la kitaifa lililotokea basi ni vema kama kungekuwa na majadiliano
ya kitaifa na wadau wahusika mapema ili kuepusha kutokea kwa vurugu au
shida katika jamii.
Mkazi wa Sakina, Samuel Mollel, alisema hauli hiyo ikitekelezwa
italeta vurugu kubwa katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu.
DK. BANA: WAZIRI KAKURUPUKA
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk. Benson Bana, alisema
inaonyesha waziri alikurupuka bila kushauriana na kwamba siyo kauli
inayopaswa kutolewa kwa umma katika zama hizi za demokrasia na siasa
huria.
“Amekosea, ninachojua serikali haiwezi kufuta Katoliki au KKKT,
utajiridhisha umewafutia, lakini dini itaendelea kuwapo, askofu hawezi
kufuta ukatoliki wangu, hayo yanatokea kwenye mataifa yenye udikteta
pekee,” alisema.
Alisema kwa kipindi hiki ambacho waziri alipaswa kusisitiza ni
vyama hivyo kuzingatia masharti ya uandikishaji wake bila kutaja siasa.
“Kuanza kusema utavifuta wakati unaona kuna tamko la maaskofu
ambalo bado lipo hai ni kujikanganya…akija kwa visivyofuata sheria na
Katiba atafikiriwa vibaya,” alisema na kuongeza:
“Ninachoona waziri ali ‘over step’ hakujiridhisha, ndiyo maana
serikali zote zinakuwa na msemaji mmoja na siyo kukurupuka, ukishasema
unafuta taasisi za dini ni hatari…natoa ushauri wa bure kwa serikali
yangu,” alisema.
Mhadhiri mwingine wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Bashiru Ally,
alisema: “Jukumu kubwa la serikali yoyote ni katika ‘law and order’ na
‘stability’, lakini serikali ya kidemokrasia haitumii mabavu bali
unaweza kujenga amani na utulivu kwenye nchi kwa kujadiliana,” alisema.
Alisema kama zipo sababu za msingi ni vyema mahakama ikatumika
kuthibitisha tuhuma zozote kwa kuwa ndicho chombo cha kikatiba chenye
uwezo wa kitaalamu wa kusikiliza na kwamba kufuta hivi hivi ni kurudi
katika utawala wa kiimla.
THRDC: TANZANIA YA SASA SIYO YA ZAMANI
Mtaribu wa Mtandao wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), Onesmo
Olengurumwa, alisema viongozi wawe makini na kutambua kuwa Tanzania ya
sasa siyo ya zamani na kwamba wanapoona mambo hayaendi lazima
wazungumze.
Alisema asasi na viongozi wa dini wana wajibu kwenye masuala yote
kwa kuwa walishirikishwa kwenye mchakato na Bunge la Katiba, hivyo kwa
sasa wanapoona mambo hayako sawa wanapaza sauti.
Alitolea mfano suala la uandikishaji wa wapiga kura kwenye Daftari
la Kudumu la Wapigakura kwa mfumo wa BVR na mchakato wa kura ya maoni
yalikuwa hayakwepeki kuzungumzia kwa kuwa amani ya nchi inategemea
masuala yote hayo.
DODOMA: CHIKAWE ASITUMIE VIBAYA NAFASI YAKE
Mkuu wa Kanisa la Anglikana Tanzania, Dk. Jacob Chimeledya, alisema
Waziri huyo asitumie nafasi yake kuchafua zaidi ila kama ni kumsaidia
basi Mungu ambariki na wanamuombea.
"Kama atafuta kwa mujibu wa sheria na taratibu na si kama
analipuka, atatekeleza kazi yake kwa usahihi, lakini akilipuka anaweza
kuleta athari kubwa,” alisema.
Alisema hofu yake ni kusiwe na hasira na zikaelekezwa kwa watu wasio na hatia.
"Viongozi wa dini tuna haki kuelekeza watu kitu gani
tunachokifikiri ambacho ni sahihi kwa hiyo kama kuna mtu akitokea akaona
ni uasi au si uasi ila na sisi pia tumepewa majukumu ya kumwambia mtu
afanye kitu gani ambacho ni sahihi,” alifafanua.
"Hebu tujiulize kwanini huko nyuma haikuwa hivi kwanini hizi hoja
kwa sasa zinajitokeza, kwanini leo hii viongozi wa dini wafike kutoa
kauli hiyo je, walikuwa ‘right’ au ‘wrong’, haya yanatakiwa kufanyiwa
utafiti na ni utafiti rahisi sana,” alisema.
Mwenyekiti wa Chama cha Ukombozi wa Umma (Chaumma) mkoa wa Dodoma,
Kayumbo Kabutari, alisema Chikawe anadanganya wananchi, nchi haiko
salama.
MAASKOFU: TUNASUBIRI WARAKA WA SERIKALI
Askofu wa Kanisa la Tanzania Assemblies of God Kanda ya Kaskazini
na Kati, Christopher Madilu, alisema tamko ni gumu kueleweka kwa sasa,
ingawa viongozi wa dini pamoja na kanisa hilo wanasubiri waraka wa
serikali ili watoe msimamo wao.
“Kuna ugumu wake katika kuzungumzia utekelezaji wa tamko la Waziri
Chikawe. Sisi tunasubiri waraka wa serikali unaoonyesha kusudio hilo,
halafu ndiyo tuzungumze ya kwetu. Lakini mpaka sasa hakuna waraka
ulioletwa, inawezekana labda serikali imechunguza na ikaona kuna makosa,
hatuwezi kujua kwa hiyo tunasubiri,” alisema Askofu Madilu.
Askofu Mstaafu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT),
Dayosisi ya Kaskazini, Dk. Martin Shao, alisema hawana taarifa na
wanasubiri waraka wa serikali.
Prof. Willy Makundi ambaye ni mtaalamu wa mabadiliko ya tabia nchi,
alisema anashangazwa na tamko hilo wakati nchi inaongozwa kwa misingi
ya sheria na Katiba.
“Hata kama kungekuwa na mtu au kikundi cha watu au taasisi ya dini
imevunja sheria, serikali haina nguvu ya kikatiba na ya kiutekelezaji
kuyafunga makanisa, isipokuwa mahakama peke yake, kwa sababu ndiyo
dalali mkuu wa haki…hakupaswa kutoa vitisho na badala yake angeagiza
waburuzwe mahakamani,” alisema Prof. Makundi
TANGA: SERIKALI IACHE VITISHO
Baadhi ya wadau wa masuala ya maendeleo mkoani Tanga wameitaka
serikali kuacha kutoa vitisho kwa raia wake kwani ni kukiuka Katiba ya
nchi kuhusiana na uhuru wa wananchi wa kutoa maoni yao bila kuingiliwa.
Walisema kauli hiyo inaweza kuchangia kusababisha vurugu ndani ya
nchi hasa kwa serikali kutaka kutumia mabavu kufanya maamuzi ambayo
hayakubaliki, jambo ambalo ni kinyume cha misingi ya utawala bora.
“Utawala bora ni ule unaofuata misingi ya haki na sheria kwa mujibu
wa Katiba ya nchi, kama Katiba inayotumika sasa inatambua uhuru wa
mwananchi wa kutoa maoni bila kuingiliwa iweje serikali ione ni kosa la
jinai,” alisema Mbone Herman, mwanafunzi wa Chuo Kikuu Huria (OUT).
Mariam Said, mkazi wa jijini Tanga, alisema kauli ya serikali
inatokana na ukweli kwamba Katiba inayopendekezwa si maoni na mahitaji
ya Watanzania, bali ni pendekezwa kwa ajili ya kuwalinda baadhi ya
waliopo madarakani.
MNYIKA: NITAPELEKA HOJA BUNGENI
Naibu Katibu Mkuu Chadema Bara, John Mnyika, alisema Chikawe
angewambia ukweli vyama wanavyotaka kuvifuta ni ambavyo walitangaza
kwenye vyombo vya habari na siyo vilivyotoa msimamo katika kura ya maoni
na uchaguzi mkuu.
Alisema iwapo vyama hivyo vitafutwa kwa kisingizio hicho atapeleka hoja bungeni lijadiliwe na waziri awajibishwe.
“Namtaka waziri asijiingize kwenye hatari ya kupelekewa hoja ya
kukiuka haki ya kikatiba ya watu kitaasisi kutoa maoni, kama ni suala la
watu kutimiza masharti ya kisheria asifute, akifuta nasi tunakwenda
kumfuta bungeni,” alisema Mnyika ambaye pia ni Mbunge wa Ubungo.
“Amekurupuka akasome vizuri Sheria ya Kura ya Maoni ajue ni haki ya
watu kushiriki kampeni na kama kura ingekuwa Aprili 30, mwaka huu,
kungekuwa na kampeni za ndiyo na hapana,” alisema.
Alisema kauli ya Chikawe na nguvu aliyotumia siyo kura ya maoni
pekee, bali wamegundua asasi, taasisi na watu wanataka mabadiliko
hawakubaliani na mfumo wa utawala, wanatoa lugha za ukali kuwatisha,
kuwaziba midomo kuelekea watu kusaka mabadiliko.
Alisema wanaosababisha kuvunjika kwa amani ni uongozi dhaifu
unaoshindwa kusimamia ufisadi na kwamba kinachoonekana kwa sasa ni
kuporomoka kwa hali ya maisha ya wananchi na tofauti kubwa kati ya
maskini na tajiri ambalo ndilo tishio kubwa.
KANDA YA ZIWA WAMSHANGAA CHIKAWE
Wakazi wa Shinyanga, walisema tamko la Chikawe ni la kukurupuka
kutokana na Katiba ya nchi kusema kila mtu ana haki ya kutoa maoni na
mawazo yake bila kuvunja sheria za nchi.
Hassani Baruti, mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo
(Chadema) wilaya ya Shinyanga Mjini, alisema Chikawe amevunja Katiba ya
nchi kwa kuingilia uhuru wa mtu binafsi na haiwezekani kuzuia watu kutoa
maoni.
Mwanaharakati wa siasa mjini Shinyanga, Saguda Komanya, alisema
kila nchi ina miongozo yake na katika suala la Katiba inayopendekezwa
kila mtu ana wajibu wa kuikosoa na kuitolea maoni.
Komanya alisema suala la hofu ya amani kuelekea uchaguzi mkuu
halipo isipokuwa Jeshi la Polisi linatakiwa lisiegemee upande wa chama
chochote zaidi ya kutenda haki.
Mkoani Simiyu, baadhi ya asasi zimeleeza kushangazwa na tamko hilo na kulitiliwa hofu.
Mwenyekiti wa mtandao wa asasi za kiraia wilayani Maswa, Nicodemas
Lutta, alisema kitendo cha Chikawe kutoa tamko hilo ni kuwanyima
wananchi pamoja na asasi zao haki ya kidemokrasia ya kuamua mambo
nchini.
Alisema kuzifungia asasi za kiraia na kidini kuna utaratibu wake,
na kumtaka Chikawe atoe ushahidi wa asasi zinazotuhumiwa kuliko
kujumuisha asasi zote hususani zile za kidini.
Lutta alisema haiwezekani kutenganisha siasa na dini na kuhoji
serikali imekuwa ikiwahimiza viongozi wa madhehebu ya dini kuhubiri
amani na upendo hasa kuelekea uchaguzi mkuu na kuwahimiza wananchi wao
bila kujali imani zao za kidini kuipigia kura ya ndiyo katiba
inayopendekezwa.
“Kwanini nawakataza wasihamisishe kupigia kura ya hapana wakati Katiba ni ya wananchi?” alihoji.
Wilayani Chato baadhi ya viongozi wa madhehebu ya dini, walisema
ni lazima kauli hiyo aifute kwani inaweza kusababisha machafuko.
“Chikawe lazima atambue viongozi wa dini ni walinzi wakubwa wa
amani nchini, hivyo kitendo cha kuwataka kuwazuia kutoa maoni yao wakati
muelekeo wa nchi unaenda mrama hakiwezekani,” alisema mchungaji wa
kanisa Anglikana Chato, Zacharia Samson.
Katibu wa Chadema wilayani Chato, Mange Ludomya, alisema Chikawe
amekiuka katiba ya nchi kwa kumkataza mtu kutoa maoni yake bila kuvunja
sheria za nchi.
“Hivyo ni vitisho ili kuwafanya wananchi waikubali Katiba
inayopendekezwa isiyoonyesha dira kwa Watanzania katika miaka 50 ijayo,”
alisema Emmanuel Magida mkazi wa Igoma, jijini Mwanza.
Edward Mboje mdau wa asasi za kiraia, alisema waziri huyo hakutumia
busara katika tamko lake hilo kwani asasi siyo serikali bali ni
wananchi, hivyo haina haja kutoa kauli inayowanyima wananchi haki ya
kutoa maoni kwa mambo ya kisimingi.
Imeandikwa na Salome Kitomari (Dar), John Ngunge na Cynthia
Mwilolezi (Arusha), Marco Maduhu (Shinyanga), Happy Severine na Anceth
Nyahore (Simiyu), Daniel Limbe (Chato) na Kisiroti Zacharia (Mwanza),
Augusta Njoji (Dodoma), Godfrey Mushi (Moshi), Lulu George na Steven
William (Tanga)
CHANZO:
NIPASHE
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
0 comments:
Post a Comment