Home » » TNBC:MIKOA IWEKE VITUO KUSAIDIA WAWEKEZAJI

TNBC:MIKOA IWEKE VITUO KUSAIDIA WAWEKEZAJI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

Baraza la Taifa la Biashara (TNBC) limeyashauri mabaraza ya biashara ya mikoa ya nyanda za juu kusini kuanzisha vituo vitakavyotoa huduma za pamoja ili kukuza uwekezaji katika maeneo yao.
Ushauri huo ni moja ya mapendekezo yaliyotolewa katika kongamano la uwekezaji lililomalizika mjini Mbeya hivi karibuni, ambapo mikoa na halmashauri zake zilitakiwa kuanzisha vituo vya kuwawezesha wawekezaji kupata vibali, leseni na huduma zote zinazohitajika katika eneo moja.
Katibu Mtendaji wa TNBC, Raymond Mbilinyi alitoa ushauri huo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa wakati wa kongamano hilo.
Alizitaka mamlaka za Serikali za Mitaa zijenge mazingira wezeshaji na zisiwe vikwazo kwa uwekezaji ili kuharakisha maendeleo.
“Kila kanda au mkoa uainishe sifa za kipekee za uwekezaji kulingana na hali halisi kiuchumi, kijamii na kijiografia kwa ustawi wa wananchi wake na kuondoa umaskini,” alisema.
Aliitaka mikoa hiyo kuhamasisha uwekezaji wa viwanda vya kusindika mazao ya kilimo na mifugo ili kuongeza thamani na kuleta tija katika uzalishaji.
“Mikoa hii ihamasishe matumizi sahihi ya pembejeo na zana za kilimo kwa lengo la kuongeza uzalishaji wa mazao hayo ya kilimo,” alisema.
Katika kongamano hilo, Serikali iliwataka wawekezaji wa ndani kuangalia ni namna gani wanaweza kunufaika na shughuli za Kituo cha Uwekezaji nchini (TIC) na kuondokana na dhana potofu kuwa kituo hicho ni cha wawekezaji wa nje pekee.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Uwekezaji na Uwezeshaji, Dk Mary Nagu alisema kuna wawekezaji wengi wa ndani ambao wamefanya uwekezaji mkubwa katika mikoa ya kusini wanaostahili kupata hadhi ya uwekezaji mahiri, lakini hawajapata nafasi hiyo.
“Kwa kutokujua ni kwa jinsi gani Kituo cha Uwekezaji kinatoa vivutio kwa wawekezaji wenye hadhi, hawakupata kutumia fursa hiyo kama ilivyotarajiwa,” alisema waziri huyo.
Takwimu zilizopo zinaonyesha kuwa katika kipindi cha mwaka 1997 hadi Machi 2014, miradi 220 iliandikishwa katika mikoa ya kanda hiyo, ikiwa na thamani ya Dola za Marekani 4 bilioni na inatazamiwa kuleta ajira 36,191.
Chanzo:Mwananchi
Jika Anda menyukai Artikel di blog ini, Silahkan klik disini untuk berlangganan gratis via email, dengan begitu Anda akan mendapat kiriman artikel setiap ada artikel yang terbit di Creating Website

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Rukwa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa