Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Habari kutoka ndani ya kamati hiyo zinasema
tofauti na fikra za wajumbe wengi kwamba mjumbe huyo angewaunga mkono
kwa kila jambo, hali imekuwa tofauti kwani amekuwa na misimamo kama
iliyoonyeshwa na wajumbe wa Ukawa ambao wamesusia Bunge hilo.
“Yule bwana pamoja na mjumbe mmoja hivi kutoka
kundi la 201 upande wa Zanzibar wametuhenyesha sana maana misimamo yao
ni ileile ya Ukawa, yaani wameamua kuandika maoni ya wachache, jambo
ambalo awali hatukulitarajia,” alisema mmoja wa wajumbe.
Gazeti hili limebaini kuwa mbunge huyo kutoka
Zanzibar ni Adil Mohamed Ali ambaye pamoja na Arfi wameamua kuandika
maoni ya wachache kuhusu eneo la madaraka ya Rais lililokuwa
likibishaniwa.
Kanuni ya 32 (10) inatoa fursa kwa wajumbe
wasiokubaliana na uamuzi kwenye kamati kuandika maoni ya wachache na
maoni hayo yamepewa dakika 60 (saa moja) kusomwa bungeni kwa mujibu wa
Kanuni ya 33 (5).
Juzi, Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo namba 10,
Salim Awadhi Salim akizungumza na waandishi wa habari alisema
walilazimika kuweka kando ibara za 72 na 73 ambazo zinazungumzia mamlaka
ya Rais wa Jamhuri ya Muungano baada ya kutokea mvutano makali.
“Sura namba saba ibara ya 72 na 73 ambayo
inahusiana na uongozi tuliahirisha ili wajumbe waweze kutafakari,”
alisema Salim huku akifafanua kwamba wajumbe wengi walisema kuwa
majukumu aliyopewa Rais katika Katiba ya sasa ni mengi, hivyo
apunguziwe.
Habari kutoka ndani ya kamati hiyo zimesema mbali
na madaraka ya Rais, suala jingine lililozua mvutano likimhusisha Arfi
na Ali ni pendekezo la wajumbe wa kamati hiyo kutaka uwapo wa makamu
watatu wa rais.
“Kulikuwa na pendekezo kwamba tuwe na makamu wa
rais watatu ambao ni yule anayetokana na mgombea mwenza, Rais za
Zanzibar ambaye anakuwa makamu wa pili na makamu watatu anakuwa Waziri
Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” kilisema chanzo chetu.
Habari zinasema kutokana na hali hiyo, Arfi na Ali
waliibua hoja kwamba ikiwa kuna pendekezo la makamu watatu wa rais, kwa
nini pendekezo la serikali tatu linakataliwa na hapo ndipo mvutano
ulipoanzia na kusababisha mjadala mkali uliochukua takriban saa nzima.
Alipoulizwa jana, Arfi hakuwa tayari kuzungumzia
suala hilo kwa maelezo kwamba kama kuna chochote kitakachotakiwa
kufahamika basi kitawasilishwa bungeni baada ya kamati kumaliza kazi
yake.
“Mimi sidhani kama ni busara kuzungumza kwa sasa,
kuweni na subira maana mahali sahihi pa kusemea mambo haya ni kule
bungeni,” alisema Arfi ambaye ameingia katika mgogoro mkubwa na chama
chake kutokana na kukiuka makubaliano ya kususia vikao hivyo.
Kwa upande wake, Ali hakuthibitisha wala kukanusha kuwapo kwa
mpango wa kuwasilisha maoni ya wachache, lakini akasema asingeweza
kuzungumza kwani alikuwa na kazi nyingi ndani ya kamati.
Habari kutoka ndani ya kamati hiyo pia zilisema
kuwa wajumbe hao wawili wamekuwa wakivutana na wenzao pale kunapotolewa
mapendekezo ya kufutwa kwa maneno ‘shirikisho’ au ‘Tanganyika’.
“Hoja yao ni kwamba kwa nini tufute maneno hayo wakati Bunge Maalumu halijaamua kuhusu muundo wa muungano?
Tumekuwa kwenye wakati mgumu kweli na katika baadhi ya ibara tumeacha hivyo,” kilifafanua chanzo chetu.
Chanzo;Mwananchi
Chanzo;Mwananchi
0 comments:
Post a Comment